Ukraine na Urusi: Kikosi kipya cha mamluki kinachoajiriwa nchini Urusi kwa vita vya Ukraine - KABATA

This is the special room for news where you need to settle with!


Breaking

Sunday 13 March 2022

Ukraine na Urusi: Kikosi kipya cha mamluki kinachoajiriwa nchini Urusi kwa vita vya Ukraine

 

Mwanachama wa Wagner katika eneo la Donbas mwaka wa 2014/15.

CHANZO CHA PICHA,@RSOTM TELEGRAM GROUP

Nchini Urusi, idhaa za mitandao ya kijamii na vikundi vya ujumbe vya binafsi vinatumiwa kuajiri kikosi kipya cha mamluki kupigana nchini Ukraine na jeshi, BBC imebaini.

BBC ilizungumza na askari mamluki na mpiganaji wa zamani ambaye alikuwa na uhusiano wa karibu na shirika moja kuu la mamluki nchini Urusi, ambaye alishiriki maelezo ya harakati za kuajiri.

Mamluki huyo alisema kwamba maveterani wengi wa shirika la siri la Wagner waliwasiliana katika kikundi cha binafsi cha Telegraph wiki chache kabla ya kuanza kwa vita.

Mengi zaidi unayoweza kusoma

Walialikwa kwenye "tafrija ya Kiukreni", na marejeleo yalifanywa kuonja "Salo", mafuta ya nguruwe ambayo yanaliwa huko Ukraine.

Ujumbe huo unatoa wito kwa "wale walio na rekodi za uhalifu, madeni, waliopigwa marufuku kutoka kwa vikundi vya mamluki au wasio na pasi ya nje" kutuma maombi.

Wanachama wa Wagner mashariki mwa Ukraine, 2014/15.

CHANZO CHA PICHA,@RSOTM TELEGRAM GROUP

Kundi la Wagner ni moja ya mashirika ya siri zaidi nchini Urusi. Rasmi, haipo: kutumika kama mamluki ni kinyume cha sheria za Kirusi na kimataifa.

Lakini wafanyakazi wapatao 10,000 wanaaminika kuwa wametia saini walau mkataba mmoja na Wagner katika kipindi cha miaka saba iliyopita.

Mhudumu wa mamluki aliyezungumza na BBC alisema wanajeshi hao wapya wanawekwa katika vitengo chini ya amri ya maafisa kutoka GRU, kitengo cha kijasusi cha kijeshi cha wizara ya ulinzi ya Urusi.

Alisisitiza kuwa sera ya uajiri imebadilika na vikwazo vichache vinatumika.

"Wanasajili mtu yeyote na kila mtu," alisema, bila kufurahishwa na kile alichoelezea kama kiwango cha chini cha taaluma ya wapiganaji wapya.

Alisema kuwa vitengo vipya vinavyoajiriwa havijulikani tena kwa jina la Wagners, lakini majina mapya yanatumika, kama vile The Hawks.

Hii inaonekana kuwa sehemu ya mtindo wa hivi majuzi mbali na sifa ya kundi la Wagner, kwani "chapa hiyo imechafuliwa," anasema Candace Rondeaux, profesa wa masomo ya Kirusi, Ulaya ya Mashariki na katika Chuo Kikuu cha Arizona State.

Wagner imekabiliwa na shutuma za mara kwa mara za ukiukaji wa haki za binadamu na uhalifu wa kivita katika operesheni zake nchini Syria na Libya.

Vyanzo vya mamluki vilivyozungumza na BBC vilisema kuwa wanajeshi hao wamefunzwa katika kambi ya Wagner iliyoko Mol'kino, kusini mwa Urusi, karibu na kambi ya jeshi la Urusi.

Tangazo la mamluki lililotafsiriwa kwa Kiingereza kwenye tovuti ya mitandao ya kijamii ya VK.

CHANZO CHA PICHA,VK SOCIAL MEDIA SITE

Mbali na vikundi vya ujumbe wa binafsi, pia kumekuwa na kampeni ya Umma nchini Urusi kuajiri mamluki.

Kwenye mtandao wa kijamii wa VK wa Urusi, ukurasa unaojieleza kama mtaalamu wa shughuli za usalama ulichapisha tangazo katika wiki ya kwanza ya uvamizi huo likiwataka "walinzi" kutoka nchi nyingine za uliokuwa Muungano wa Sovieti kutuma maombi. kwa "mgeni wa karibu".

Wataalamu wa kijeshi wanadai kwamba hii ni kumbukumbu ya Ukraine.

Hapo awali, rekodi za uhalifu zilikuwa kikwazo kwa wale waliotaka kujiunga na mamluki.

Vizuizi pia vimewekwa kwa mtu yeyote aliyezaliwa nje ya Urusi kwa sababu ya maswali ya uaminifu.

Kuna "mahitaji makubwa ya wapiganaji" na kuleta mabadiliko "utahitaji maelfu ya mamluki," anasema Jason Blazakis, mfanyakazi mwandamizi katika Kituo cha Soufan, Taasisi ya usalama yenye makao yake makuu nchini Marekani.

Siku ya Ijumaa, Waziri wa Ulinzi wa Urusi Sergei Shoigu alisema kuwa wapiganaji 16,000 kutoka Mashariki ya Kati walijitolea kupigana kwa ajili ya jeshi la Urusi.

Uwepo Ukraine

Rais wa Urusi Vladimir Putin alitoa amri kuruhusu wapiganaji wa Mashariki ya Kati kutumwa katika vita.

Hadi wapiganaji 400 wa kundi la Wagner wameripotiwa kuwa nchini Ukraine.

Kundi la Wagner lilitambuliwa kwa mara ya kwanza mwaka wa 2014, wakati lilikuwa likiwaunga mkono watu wanaounga mkono Urusi kujitenga katika mzozo wa mashariki mwa Ukraine.

Mpiganaji huyo wa Wagner alieleza kuwa katika siku za kwanza za uvamizi wa Ukraine alitumwa katika jiji la pili kwa ukubwa nchini humo, Kharkiv, akibainisha kuwa kikosi chake kilikamilisha misheni huko bila kufichua ilikuwa ni nini.

"Kisha walitulipa $2,100 kwa kazi ya mwezi mmoja na tukarudi nyumbani Urusi," aliambia BBC.

Wafuasi wa Wagner nchini Syria.

CHANZO CHA PICHA,@RSOTM TELEGRAM GROUP

Blazakis anaelezea matumizi ya mamluki kama "ishara ya kukata tamaa" kudumisha uungwaji mkono wa umma wa Urusi.

Uvamizi wa Putin nchini Ukraine umezusha maandamano kadhaa nchini Urusi. Maelfu wamekamatwa.

Blazakis aliongeza kuwa matumizi ya mamluki yanaruhusu Kremlin "kuweka idadi ya vifo chini kwa sababu mamluki hutumiwa kama chambo."

Moscow imekataa kila mara uhusiano wowote na vikundi vya mamluki.

BBC iliuliza Wizara ya Ulinzi ya Urusi ikiwa kambi ya Mol'kino inatumiwa kuajiri vikosi vya ziada kwa kile mamlaka ya Urusi inaita "operesheni maalum ya kijeshi nchini Ukraine". Hakuna jibu lililopokelewa.

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad

Responsive Ads Here